Mto Mara: Kiungo cha Maisha Yetu, Urithi Wetu

Na; Evaristy Masuha

Kwa familia nyingi, Mto Mara ni maisha. Unanywesha mifugo , unawasaidia kwenye kilimo, na unawawezesha kuendesha maisha yao ya kila siku. Kwa watoto, mto huu ni darasa la asili wanajifunza kuogelea, kuvua samaki, kuwaona ndege na miti ya asili. Kwa watalii wanaomiminika kila mwaka Serengeti, ni jukwaa la kushuhudia maajabu ya dunia: Nyumbu na Pundamilia maelfu wakivuka maji kwenda Kenya.

Ni nyumbu hao ambao wanatajwa kwenda nchini Kenya ambako wanaanzisha mahusiano ambayo yanazalisha mimba, kisha wanavuka kurudi Tanzania kuzaa na kuanza malezi ya watoto.

Mto Mara unapita katika nchi mbili: Kenya na Tanzania. Unaanzia katika Safu ya Milima ya Mau nchini Kenya, unapitika kwenye Hifadhi ya Wanyamapori ya Maasai-Mara nchini Kenya na Hifadhi ya Taifa ya Serengeti nchini Tanzania, hatimaye kumwaga maji yake katika Ziwa Victoria.

Mto huu umekuwa kiungo cha ushirikiano wa mataifa ya Tanzania na Kenya, ukiimarisha Diplomasia ya Uchumi, mshikamano wa kijamii na kitamaduni. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, mara kwa mara amesisitiza umuhimu wa kuyatumia maji kama chachu ya kudumisha mahusiano ya kikanda na kimataifa.

Kwa mwaka huu wa 2025 kuanzia Septemba 13–15, mataifa haya yanayounganishwa na Mto Mara yatakutana mjini Butiama, chini ya kaulimbiu “Hifadhi Mto Mara: Linda Uhai.” Haya si maadhimisho au sherehe tu. Ni nafasi ya watu kujiuliza swali muhimu: Kama sisi ttulivyourithi, tutauachaje mto huu kwa vizazi vijavyo?

Maadhimisho ya 14 ya Siku ya Mto Mara, yanaandaliwa kwa ushirikiano kati ya Wizara ya Maji na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara.

Septemba 15 imekuwa ikiheshimiwa kila mwaka kama Siku ya Mto Mara, ikihusiana moja kwa moja na tukio la kihistoria la msafara wa nyumbu wanaovuka Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, Tanzania, kuelekea Hifadhi ya Maasai-Mara nchini Kenya, na kurejea tena Serengeti. Tukio hili limekuwa kivutio kikubwa cha utalii duniani, likiibua heshima kubwa kwa Tanzania kama kitovu cha utalii wa asili.

Mto Mara pia ni chanzo kikuu cha maji katika Ziwa Victoria, ziwa kubwa la maji baridi barani Afrika na la pili kwa ukubwa duniani. Maji yake yananufaisha nchi za Tanzania, Kenya na Uganda kwa upande wa Afrika Mashariki, yakiendelea kusafiri hadi nchini Misri katika Bahari ya Mediterania kupitia Mto Nile.

Chanzo cha Mto Mara ni chemichemi za Enopuyapui katika Milima ya Mau nchini Kenya, na huchukua eneo la kilomita za mraba 13,504, ambapo asilimia 65 ipo Kenya na asilimia 35 ipo Tanzania.

Zaidi ya kuwa mhimili wa uhai kwa binadamu, mifugo na wanyamapori, Mto Mara umekuwa kichocheo cha uchumi kupitia kilimo, uvuvi na utalii. Watafiti wanabainisha kuwa bila uhifadhi thabiti wa mto huu, maisha ya mamilioni ya watu na viumbe hai katika ikolojia ya Mara-Serengeti yangetumbukia hatarini.

Kutambua uzito huo, Serikali ya Tanzania imeamua mwaka huu kuyaunganisha maadhimisho ya Siku ya Mto Mara na Mkutano wa Kimataifa wa Wanasayansi wa Maji (International Maji Scientific Conference) unaoratibiwa na Chuo cha Maji. mkutano huu utawaleta na kuwakutanisha pamoja wataalamu kutoka duniani kote kujadili tafiti na masuala muhimu yanayohusu maji, ili kupata suluhisho la kitaalamu.

Aidha, shughuli za upandaji miti rafiki wa maji zimepangwa katika maeneo mbalimbali kama njia ya kulinda vyanzo vya maji na kuimarisha uendelevu wa ikolojia. Pia, michezo na mashindano mbalimbali yatafanyika ili kuhamasisha jamii kushiriki moja kwa moja katika uhifadhi wa rasilimali hii adhimu.

Dkt. Masinde Bwire wa Kamisheni ya Bonde la Mto Nile anasema Siku ya Mto Mara ni jukwaa la kutambua na kulinda uhai wa mfumo ikolojia wa Mara-Serengeti. Ni jukwaa la kutambua kwamba kila tone la maji lina umuhimu kwa binadamu na mnyama anayelitegemea, Pamoja na ikoljia yote kwa ujumla.

Kwa upande mwingine, Tanzania imedhihirisha uongozi imara ndani ya Kamisheni ya Bonde la Ziwa Victoria, ikishirikiana na nchi Tisa wanachama ambazo ni Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Sudan Kusini, Somalia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Ushirikiano huu umenufaisha miradi mikubwa ukiwemo ule wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA) jijini Mwanza kupitia Programu ya Pamoja ya Usimamizi na Uendelezaji wa Rasilimali za Maji katika Bonde la Ziwa Victoria (LVB-IWRM), wenye thamani ya zaidi ya Shilingi bilioni 12.6. Mradi huu unalenga kujenga miundombinu ya majitaka na usafi wa mazingira  jijini Mwanza

Rais wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameendelea kusisitiza kuwa uhifadhi wa rasilimali za maji ndio msingi wa mshikamano wa kikanda na ustawi wa kijamii. Ni kupitia juhudi kama hizi Tanzania imejipambanua si tu kama taifa la hifadhi ya wanyamapori, bali pia taifa la uhifadhi wa uhai.

Aidha, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, ameweka msimamo wa wazi kuwa Wizara haitasita kuchukua hatua kali kwa yeyote atakayehatarisha usalama wa Mto Mara akisisitiza kuwa mto huu ni tegemeo la maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa maelfu ya wananchi, na ndio msingi wa mustakabali wa utunzaji wa mazingira na uhakika wa huduma ya majisafi na salama nchini Tanzania.

Wakati watalii wakipiga picha za nyumbu wakivuka, tumkumbuke mama wa Kijiji cha Kirumi, anayehitaji huduma ya majisafi na salama kwa matumizi ya nyumbani, Tumkumbuke mvuvi kutoka Kijiji cha Manga ambaye pato la familia yake linatokana na mto Mara. Tumkumbuke Mtoto kutoka kitongoji cha Makora anayeogelea kandokando ya mto. Wote hawa wanashuhudia kwamba Mto Mara ni zaidi ya maji, Mto Mara ni uhai.

Kwa mantiki hiyo, uhifadhi wa Mto Mara si hiari bali ni wajibu wa kizazi chetu. Ni njia ya kulinda urithi wa asili, kuchochea uchumi, kuzuia mafuriko na kukabiliana na changamoto za upungufu wa maji.

Hifadhi Mto Mara: Linda Uhai.
Twendeni Mara. Twendeni Butiama.

Ni Tarehe 13-15, 2025

 

 

 

 

Comments

Popular posts from this blog

Ujenzi wa Mabwawa kusaidia kuondoa changamoto ya maji Dodoma

Wataalamu Sekta ya maji shirikishaneni maarifa – Naibu Waziri Maji

Katibu Mkuu Wizara ya Maji asisitiza matumizi ya mfumo wa taarifa za sekta ya maji (Maji App)