Hongera sekta ya maji kuwa namba moja Duniani 2023.

 Na Evaristy Masuha.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ridhaa yake mwenyewe aliamua kujiwekea utaratibu wa kutoa zawadi ya fedha taslimu kwa washindi wa mashindano mbalimbali ya soka ambayo yanashirikisha timu ya taifa na vilabu vyote vya hapa nchini.

Zawadi hizi zinazotolewa kutokana na idadi ya magoli yaliyopatikana katika mechi husika za kimataia. Hili limekuwa likifanyika kwenye mechi za kimataifa ambapo wanufaika wakuu wamekuwa ni timu ya Taifa ya Tanzania pamoja na timu kongwe za Simba na Yanga ambazo hadi sasa zinashiriki mashindano ya Klabu Bingwa Barani Afrika.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akikinga maji katika moja ya miradi aliyoizindua mwaka 2023

Wakati Rais Samia akiwapima na kuzizawadia timu zake za hapa nchini, upande wa Sekta ya Maji Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inaongozwa na Mhe. Rais Samia inapimwa na kupambanishwa na mataifa mbalimbali katika kunufaika na fedha zinazotolewa na Benki ya Dunia.

Fedha hizo zinavunwa kupitia Progam ya Endelevu ya Usambazaji Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (SRWSSP) ambapo wanufaika wa eneo hili wanalipwa kutokana na matokeo ya mradi uliotekelezwa. Mpango huu maarufu kwa jina la Lipa kwa Matokeo (PforR). 

Tenki la maji lililotekelezwa kupitia fedha za PforR

Kupitia PforR, Benki ya Dunia hutoa fedha na kufanya ufuatiliaji. Uwezekano wa kuongezewa fedha zaidi unatokana na idadi ya watu ambao nchi husika imeweza kuwafikishia huduma ya majisafi wananchi wake. Idadi kubwa ya watu uliowafikishia huduma vinaamua kiwango cha fedha unachostahili kupata ili kuendelea kuwafikia wanufaika zaidi.

Kwa vile mavuno ya fedha husika yanatokana na huduma katika Sekta ya Maji ni wazi msimamizi mkuu wa eneo hili, aliyeaminiwa na Rais Samia ni Waziri wa Maji. Ingekuwa kwenye soka huyu ndiye Kocha Mkuu aliyeamiwa na timu husika kukamilisha mipango na ushindi. Hivyo, Waziri wa Maji anafanikisha hitaji la bosi wake Rais Samia kuhakikisha anakimbizana na utekelezaji wa miradi bora ya maji ili kuvuna zaidi fedha hizi na kupunguza machungu ya huduma ya majisafi kwa wananchi.

Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso akijiridhisha na ubora wa maji katika moja ya mradi wa maji kabla ya uzinduzi

Ifahamike kuwa licha ya idadi ya watu uliowafikishia mradi, Benki ya Dunia inachukua hatua kujiridhisha kuhusu ubora wa mradi na uendelevu wake.

Waziri Aweso anafahamika kama shabiki wa mpira wa miguu, pamoja na michezo mingine pia na mara kadhaa amekuwa akitania watendaji wake kwamba katika kuhakikisha huduma ya maji inamfikia kila Mtanzania yeye anasimama kama Benchika, Kocha Mkuu wa Simba.

Nianze kwa kumpongeza huyu Benchika wa Sekta ya Maji kwa kufunga mwaka bila kumuangusha Bosi na wadau wake. Mhe. Aweso anafunga mwaka akitembea kifua mbele kwa kuwa namba moja kati ya zaidi ya mataifa 50 yanayoshindana katika kuvuna fedha za PforR.

Taarifa ya kuwa bingwa katika eneo hili ilitajwa na Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia, Kanda ya Mashariki na Kusini mwa Afrika, Dkt. Victoria Kwakwa katika mkutano uliohusu Maji na Usafi wa Mazingira (Wash Leadership Summit) uliofanyika Novemba 14-15, 2023, Jijini Addis Ababa nchini Ethiopia.  

Mkutano huu ambao ulikuwa ukijadili masuala mbalimbali ikiwemo utekelezaji wa mradi huo uliwahusisha mataifa mbalimbali yanayotekeleza program hii, Tanzania ikatajwa kuwa kinara wa utekelezaji wa miradi hii. Kwakwa alienda mbali kwa kuwataka mataifa mengine yajifunze kutoka Tanzania.

Mafanikio haya hayajaifanya Dunia kukaa kimya. Hata kabla ya tangazo hilo, Benki ya Dunia ilishachukua hatua ya kuyashauri mataifa mbalimbali ambayo yanakutana na changamoto mbalimbali katika utekelezaji wa miradi hiyo kuja kujifunza Tanzania.

Picha ya pamoja ya timu ya Wataalam kutoka sekta ya maji Nigeria pamoja na wenyeji wao Tanzania walipotembelea Tanzania kujifunza kuhusu utekelezaji wa miradi ya maji kupitia PforR

Miezi michache iliyopita timu ya wataalama kutoka nchini Nigeria ilikuwepo hapa nchini kwa ajili ya kupata uzoefu wa miradi hii ya P4R. Wataalam wa Sekta ya Maji kutoka Tanzania wamepata fursa ya kutembelea nchi mbalimbali duniani kushirikishana uzoefu na mafanikio. Hongereni tena wizara ya maji kwa kuendelea kuitangaza Tanzania na kuonesha kwamba Tanzania inaweza.

Wataalam kutoka Nigeria wakiwa katika moja ya mradi wa maji wilayani Manyara

Kwa mujibu wa Wizara ya Maji awali Tanzania ilifadhiliwa kwa Dola za Marekani milioni 350, takribani shilingi bilioni 823 kwa kipindi cha miaka mitano 2019/2020 hadi 2024/2025.

Ndani ya miaka mitatu, Benki ya Dunia iliridhishwa na kasi ya utekelezaji wa miradi kupitia mpango huo ambapo Tanzania ilikuwa imefikisha maji kwa zaidi ya watu wapya milioni 4.7 kwa mikoa 17. Licha ya kufikisha huduma ya majisafi kwa wanufaika Benki ya dunia ilijiridhisha kwamba miradi iliyotekelezwa kupitia mpango huo ilikuwa na ubora unaostahili katika viwango vya kimataifa.

Kutokana na matokeo hayo Benki ya Dunia imeiongeza Tanzania Dola za Marekani milioni 300. Licha ya hivyo,  imeiruhusu Tanzania kupanua wigo wa utekelezaji wa miradi kutoka mikoa 17 hadi kufikia mikoa 25.  

Mafanikio haya yanaongeza kasi ya kufikia malengo yaliyoainishwa na Serikali kufikia mwaka 2025 huduma ya maji vijijini iwe imefikia asilimia 85 wakati mijini huduma hiyo ikiwa imefikia asilimia 95.

Naibu Waziri wa Maji Mhandisi Maryprisca Mahundi (Mb) akikagua mradi wa maji

Taarifa za Wizara husika ya Maji zinaonesha kwamba hadi wizara inafunga mwaka huduma ya maji mijini na vijijini imefikia wastani wa asilimia 81 ambapo kwa mjini ni wastani wa asilimia 88 na vijijini ni wastani wa asilimia 77. Vijiji vilivyo na huduma ya maji ni 9,259 kati ya vijiji 12,318.


 

Aidha, jumla ya miradi 506 ilikamilishwa ikiwemo 436 ya vijijini na 70 ya mijini yenye uwezo wa kuhudumia wananchi 5,754,340 (3,145,645 wa vijijini na 2,608,695 wa mijini).

Naibu Waziri wa Maji Mhandisi Maryprisca Mahundi akimtua mama ndoo ya maji

Mheshimiwa Aweso anawapa matumaini Watanzania na Dunia kwa ujumla kwamba taratibu zinaenda vizuri kwani miradi iliyopo ni mingi na itawezekana huduma hiyo kupanda kwa kiwango kikubwa. Aidha hakuna mashaka kuwa malengo ya serikali yatafikiwa na hata kuzidi.

 

Kila raheli Sekta ya Maji. kila la heri wadau wa maji. kila la heri Watanzania katika 2024.

 

Comments

Popular posts from this blog

Ujenzi wa Mabwawa kusaidia kuondoa changamoto ya maji Dodoma

Wataalamu Sekta ya maji shirikishaneni maarifa – Naibu Waziri Maji

Katibu Mkuu Wizara ya Maji asisitiza matumizi ya mfumo wa taarifa za sekta ya maji (Maji App)