Mwalimu JK Nyerere, karibu Tena Butiana. Uyaone ya Aweso
Mpendwa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Pole
kwa majukumu mapya uliyonayo huko Peponi. Lengo langu kuu ni kukupa simulizi ya
kinachoendelea katika sekta ya maji huko jimboni kwako lakini nimeona vema nianze
kukupa pole kwa majukumu mapya kutokana na Imani yangu ambayo sina hakika kama
iko sahihi kwamba kwa wachapa kazi kama wewe mnapoiaga dunia, Mwenyezi Mungu
anawapa majukumu mengine ili muendelee kuijenga jamii katika ulimwengu huo
mpya. Naomba nisamehewe kama fikra zangu haziko sahihi lakini niendelee
kuaminiwa kwamba uliondoka wakati watanzania wengi tungali tunakuhitaji
Mpendwa Baba wa Taifa. Mimi ni mtanzania mwenzako ambaye
nimekuwepo katika kipindi ukiiongoza nchi hii. Nimekuwepo nikiwa mmoja wa
wakazi wa Mkoa wa Mara katika Kijiji cha Nambaza wilaya ya Bunda. Nikiri kwamba
sikupata fursa ya kuwa miongoni mwa chipukizi uliokuwa ukituita kuja kukusaidia
kuvuna mazao yako hapo Butiama. Pengine hiyo ingenipa fursa ya kukaa karibu na
wewe na kuchota hekima yako.
Utakumbuka kwamba wakati wa mavuno ulikuwa ukituita vijana wa
chipukizi kutoka sehemu mbalimbali mkoani hapo kuja kukusaidia kuvuna mazao. Si
kwamba sikupenda kushiriki katika kazi hiyo njema isipokuwa walimu wangu
waliokuwa wakiunda vijana wa chipukizi hawakuniona kwamba nina sifa hiyo.
Wao walidhani mimi ni goigoi lakini nikuhakikishie kwamba huo
ulikuwa mtazamo wao. Mimi leo hii ni shujaa na mchapa kazi mzuri. Ukitaka
uhakika wa hili muulize kijana aliekuwa kiongozi mkuu wa Scout, Innocent Sabato
Nanzaba ambaye sasa ni Katibu wa CCM moja ya mikoa huko Unguja. Namtaja huyu
kwa sababu nafahamu alikuwa na nafasi ya kukaa karibu na wewe katika shughuli mbalimbali
wakati huo akiwaongoza vijana wote wa scouti huko Wilayani Bunda akitokea hapo
kijijini kwetu.
Mpendwa Baba wa Taifa. Licha ya kuzaliwa huko mkoani Mara katika Jimbo la Mwibara ambalo wakati huo lilikuwa sehemu ya jimbo la Bunda, nilipata nafasi ya kuishi jimboni kwako katika Kijiji ha Kiabakari wakati huo likiitwa jimbo la Musoma vijijini. Uzoefu huu na utu uzima wangu umeniwezesha kufahamu baadhi ya masahibu waliyokuwa wakiyapata wakazi wa mkoa wa mara na hasa jimboni kwako kikiwepo Kijiji chako cha Butiama. Fursa hii ndiyo inayonipa nafasi ya kukusimulia hali inayoendelea sasa baada ya miaka kadhaa tangu utuage watanzania.
Mpendwa Baba wa Taifa. Utakumbuka vizuri kwamba uliacha mradi
wa maji uliokuwa ukianzia Kijiji cha Mugango kuelekea Butiama kupitia kiabakari?
Sikuwahi kukuambia lakini leo nikusimulie kwamba malalamiko ya wananchi wa
kiabakari katika miaka hiyo ya 1990 wakati ambao ulikuwa umeshastaafu uongozi ilikuwa
ni kwamba mradi huo umechakaa wewe huchukui hatua ya kuwaambia viongozi walioko
serikalini ili wafanye haraka kuurekebisha. Jambo lililokuwa wazi ni kwamba
kweli mradi ulikuwa umechoka kwelikweli. Maji yalikuwa yakitoka mara chache
sana.
Kwa waliokuwa wakielewa msimamo wako walijipa majibu wenyewe kuwa
hiyo ni tabia yako na msimamo wako wa kutotaka kuvutia maendeleo kwenye maeneo
yako. Zaidi ulilenga maendeleo ya nchi nzima hasa kwa waliokuwa na mahitaji
zaidi. Mfano wa wazi ulikuwa Barabara ya kuja kwako kutokea barabara kuu ya
Mwanza Musoma.
Nakumbuka hadi unaiaga dunia, kutoka pale Nyamisisi
Kiabakari, tulikuwa tukikata kona kuikamata barabara ya kuja Butiama nyumbani
kwako tunaanza kukulaumu kwa nini barabara imechoka hivyo na wewe uko kimya tu.
Tulikuwa tukikuona unapita na gari lako kimyakimya tunabaki kukushangaa. Tulikuwa
tukijilinganisha na wenzetu wa mikoa ya kaskazini ambao tuliamini wana
maendeleo kwa sababu viongozi wao waliokuwa chini yako waliamua kupeleka fursa
huko kwao jambo ambalo wewe hukutaka kulifanya.
Majibu haya nilikuja kuyapata majuzi wakati nilipomsikia Mhe.
Sospeter Mhongo Mbunge wa Jimbo la Msoma vijijini akisimulia kwamba uliwahi
kumwambia kwamba wananchi wanakata mabomba na kusababisha wewe na wananchi
wengine wa Butiama wakose maji. Mheshimwa Muhongo alitoa maelezo haya
akiwaeleza wajumbe wenzake wa iliyokuwa Kamati ya Kudumu ya Bunge
inayoshughulika na maji wakati walipotembelea mradi Mpya wa maji wa Mugango-Kiabakari
Butiama. Alisema wewe ulikuwa ukiishauri serikali isilenge kufikisha maji
Butiama bila kuhakikisha wananchi wanaopitiwa na miundombinu hiyo wanapata
huduma hiyo.
Mpendwa baba yetu. Leo ni zaidi ya miongo miwili tangu
umetangulia mbele ya haki. Naomba nikupe siri kwamba sasa sekta ya maji
imempata mchezaji. Msemo wa Waswahili kwamba upele umepata mkunaji umetimia. Sasa
hivi serikali yako uliyoipenda inaongozwa na mwanamama Samia Suluhu Hassan.
Sina shaka ulimuacha akiwa ameianza siasa lakini hakuwa katika nafasi za juu
zaidi. Huyu Mama kaamua sekta ya maji kumpa bwana mdogo machachari kweli kweli anaitwa
Jumaa Hamidu Aweso.
Huyu Aweso ni Mbunge wa Pangani. Alianza kama Naibu Waziri wa
Maji akiwa chini ya Waziri Mbarawa, kisha akapewa nafasi ya uwaziri. Wakati
anapewa madaraka kulikuwa na lawama lukuki za changamoto ya huduma ya maji
sehemu mbalimbali nchini. Alipoingia madarakani tu akatangaza kuwa wizara yake
ni Wizara ya maji si Wizara ya ukame.
Akasema atahakikisha Wizara hiyo inatoka kuwa wizara ya Kero na
kuwa wizara ya kusuluhisha kero za wananchi. Akawa na kawaida ya kusimama
jukwaani anatukumbusha kitabu cha Tenzi za Rohoni, wimbo namba 22 usemao ‘Unapozuru
wengine usinipite mwokozi’. Akasema wizara yake itahakikisha haimpiti mtanzania
yeyote katika kuhakikisha anafikiwa na huduma ya majisafi na salama. Tulidhani
ni masihara ya wanasiasa lakini sasa tunayaona wazi.
Licha ya kuwa mchapa kazi ambaye hakai ofisini Kijana Aweso
amekuwa na maamuzi ya haraka ya kuhakikisha anasikia shida na vilio vya
wananchi. Hii imemfanya awe na sifa njema kwa kila jamii anayoifikia na hivyo
kuwa miongoni mwa mawaziri ambao wanasifika zaidi kwa utatuaji wa haraka wa
shida za wananchi.
Utendaji huu uliotukuka ndiyo unanipa nafasi ya kukusimulia
hilo fupa la mradi wa Mugango wa kiabakari lilikuwa likifanya wananchi
wakulaumu kwamba hujataka kulichukulia hatua. Chini ya Rais Samia kupitia waziri Aweso mradi
huo umeanza kujengwa upya kwa kuwekeza zaidi ya shilingi Bilioni 70. 5
Kile kilio chako cha kutaka wananchi wote wanaopitiwa na
mradi huo wapate huduma kimepatiwa majibu. Chini ya Waziri Aweso mradi huo
ambao unatarajiwa kukamilika Desemba mwaka huu jumla ya vijiji 39 vinavyopitiwa
na miundombinu ya mradi vitapata huduma ya majisafi. Hii itafanya wakazi
takribani 233,000 kupata huduma kupitia mradi huu ambao umesanifiwa uwe na
uwezo wa kuhudumia wananchi hadi mwaka 2040. hii inamaanisha kwamba hata
ongezeko la wananchi watakaokuwepo kwa miaka hiyo, bado wataweza kupata huduma
ya majisafi, salama na yenye kutosheleza.
Mpendwa Baba wa Taifa kwa mapenzi makubwa niliyonayo kwako
ninayo mengi ya kukusimulia jinsi nchi inavyokimbia katika masuala mbalimbali
ikwemo sekta ya maji. kwa vile leo ni siku ya kukumbuka naomba niishie hilo
moja. Siku nyingine nitakuwa na mengi yenye kukumbusha ulivyoweka misingi imara
ya uongozi wa Nchi. Upumzike kwa amani. Mpendwa Baba wa Taifa.

Comments
Post a Comment