Jamii ishirikishwe katika masuala ya maji - Aweso

Picha mbalimbali za Waziri wa Maji Mhe. Jumaa aweso akizungumza katika kikao cha mafunzo kwa Wakurugenzi na Menejimenti za Mamlaka za Majisafi na Usafi wa Mazingira.


Waziri wa Maji Mhe. Jumaa Aweso (Mb) amezindua Bodi za Mamlaka za Maji Nchini na kuwataka viongozi wa Sekta ya Maji kuhakikisha wanashirikiana na wadau wengine katika hatua mbalimbali ili kuhakikisha Sekta ya Maji inasonga mbele.

Kabla ya kuzindua Bodi hizo Mhe. Aweso amefungua kikao cha mafunzo kwa Wakurugenzi na Menejimenti za mamlaka za majisafi na usafi wa mazingira ambapo amemtaka Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji Prof. Jamal Katundu kuhakikisha bodi hizo zinakuwa mkono wa wizara na kupokea maoni mbalimbali kutoka kwa makundi mbalimbali wakiwemo viongozi wa kisiasa, viongozi wa Serikali, wafanyabiashara na watumishi wastaafu waliobobea katika masuala ya maji.

"Hatuwezi kufanya kazi peke yetu. Lazima tuhakikishe tunashirikiana na wadau wengine ili kuhakikisha tunafikia malengo tuliyojiwekea" Mhe. Aweso amesema na kuongeza kuwa lengo ni kufikia upatikanaji wa huduma ya maji vijijini kwa asilimia 85 na mijini asilimia 95, na kupita kiwango hicho ili kuwafikia wananchi “kumtua mama ndoo ya maji kichwani”.

Waziri Aweso akikagua mabanda kabla ya kikao

Amesema hivi sasa zoezi la utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maji linaendelea vizuri na jambo la kuangalia ni kuhakikisha utoaji wa huduma za uhakika na taarifa kwa wateja pale inapotokea hitililafu katika uzalishaji wa maji.

Akizungumzia suala la upotevu wa maji (NRW) amezitaka bodi kufuatilia kwa kina kuhusu mivujo na kiwango cha maji kinachopotea ili kuona uhalisia wa taarifa kwa sababu inawezekana maji yanatumika bila kulipiwa.

Mafunzo hayo yameshuhudia bodi za wakurugenzi za mamlaka za maji 25 zikizinduliwa na baadhi ya mamlaka za maji zikipandishwa madaraja kuendana na vigezo ikiwamo vya utoaji huduma na kumudu kujiendesha.

Comments

Popular posts from this blog

Ujenzi wa Mabwawa kusaidia kuondoa changamoto ya maji Dodoma

Wataalamu Sekta ya maji shirikishaneni maarifa – Naibu Waziri Maji

Katibu Mkuu Wizara ya Maji asisitiza matumizi ya mfumo wa taarifa za sekta ya maji (Maji App)