Huduma ya majisafi kutoka ziwa Victoria kusambaa vijiji vya Kishapu


Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji Mhandisi Cyprian Luhemeja akizungumza na vyombo vya habari baada ya kukagua miradi ya maji wilayani Kishapu

Mhandisi Luhemeja akikagua eneo cha chanzo cha maji cha mto Tungu wilayani Kishapu kinachotumika sasa kwa ajili ya huduma ya maji kwa wananchi wa vijiji vya  Ndoleleji
Mhandisi Luhemeja akipanda maelezo ya mradi kutoka kwa meneja wa RUWASA wilaya ya Kishapu

Moja ya tenki la mradi wa maji Masanga-Ndoleleji

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maji Mhandisi Cyprian Luhemeja, ametembelea na kukagua mradi wa maji wa Masanga-Ndoleleji,  Wilaya ya Kishapu Mkoani Shinyanga na kuridhishwa na maendeleo ya mradi huo.

Mhandisi Luhemeja amesisitiza kuwa pamoja na kazi kwenda vizuri ni muhimu kwa Mkandarasi kumaliza kazi hiyo kwa wakati Ili wananchi wapate maji kwa haraka.

"Nimeridhishwa na ubora wa miradi ya maji Wilayani Kishapu, kazi inaenda vizuri. Katika mwaka huu mpya wa fedha watapokea kiasi cha shilingi bilioni saba kutekeleza miradi ya maji" Mhandisi Luhemeja amesema

Mhandisi Luhemeja ameagiza wataalamu wa Wizara ya Maji wanaosimamia mradi huo kuhakikisha maji ya ziwa Victoria yanafika na kusambazwa kwa wananchi kupitia mradi huo kwasababu ni chanzo endelevu.

Naye Mbunge wa Kishapu Mhe. Boniphace Butondo ameishukuru Serikali kwa kuleta fedha za miradi ya maji eneo hilo huku akipongeza hatua za Wizara kutumia maji ya ziwa Victoria  kama chanzo cha kuaminika zaidi katika mradi.

Mhandisi Valeriana Tovagonze kutoka Kampuni ya Mponela Construction & Co Ltd wanaotekeleza mradi huo amesema kazi imefikia asilimia 75 na ifikapo mwezi wa Agosti 2023 wananchi wataanza kupata huduma ya  maji.

Tunashukuru kwa ushirikiano tunaopata toka Serikalini ikiwa ni noja ya kampuni za kizawa kuaminiwa katika miradi ya maji, ifikapo Agosti 16, 2023 wananchi wa Ndoleleji wataanza kupata huduma ya maji.

Mradi wa maji Masanga-Ndoleleji unagharimu kiasi cha shilingi bilioni 1.6 na umehusisha ujenzi wa matenki mawili yenye ujazo wa Lita laki 1 kila moja na utahudumia wakazi  zaidi ya 12,700 pindi utakapokamilika.

Comments

Popular posts from this blog

Ujenzi wa Mabwawa kusaidia kuondoa changamoto ya maji Dodoma

Wataalamu Sekta ya maji shirikishaneni maarifa – Naibu Waziri Maji

Katibu Mkuu Wizara ya Maji asisitiza matumizi ya mfumo wa taarifa za sekta ya maji (Maji App)