Mwisho wa Dola ya Marekani huu hapa


Rais Joe Biden wa Marekani pamoja na Rais Mstaafu wa Taifa hilo Barack Obama (Kushoto)

Nimeingia  katika maktaba yangu ya historia. Maktaba hii inahusisha yale niliyoyasoma kuanzia kidato cha kwanza hadi elimu ya Chuo Kikuuu. Nauona mwisho wa taifa linaitwa Marekani (USA). Imani yangu ni kwamba mwalimu wangu wa historia hasa aliyenifundisha kidato cha kwanza hakunidanganya kuniambia kwamba jambo lolote linaweza kuangaliwa katika mtazamo wa kihistoria. Alisema historia inasaidia kujifunza yanayotokea leo, kutokana na yale yaliyowahi kutokea. Alisisitiza kwamba elimu hiyo itanisaidia kuepuka ili nisije nikafanya makosa kama waliyoyafanya wengine. Sina shaka Mwalimu wangu Magudila Mgeta wa Bwasi Sekondari miaka ya tisini tukizoea kumuita kwa jina la utani ‘TX’ alikuwa sahihi.

Maarifa ya mwalimu TX yananipa jicho la kukitazama Kinachoendelea katika mapambano kati ya Urusi Na Ukraine. Sasa inaelekea ni vita kati ya Urusi na Washirika wake dhidi ya NATO wakiongozwa na taifa kubwa zaidi kiuchumi duniani, taifa la Marekani. Urusi naye amekataa kuwa peke yake. Amewapata wapambe wake wakiongozwa na China taifa ambalo linatajwa kukua zaidi kiuchumi duniani. Mpambano huu umeigawa dunia. kila mmoja amekuwa mtabiri. Wengine wakiutabiri mwisho wa Marekani na NATO kwa ujumla. Wengine wakiutabiri mwisho wa Urusi. Sisi yetu macho lakini maktaba yangu ya historia hainidanganyi. Inanikumbusha mengi.

USA na washirika wake wana nafasi ya kujifunza kupitia sababu mbalimbali zilizowafanya wenzao wakapotea katika ulimwengu wa mafahari wa Dunia. Shuleni tulifundishwa dola maarufu zilizobeba simulizi ya wakati huo. Dola ya Ghana, Dola ya Mali, Songhai, Dola ya Mwenemtapa. Asante na zingine nyingi.

Hizi dola ziliongozwa na watu maarufu, huko kwetu majita wanawaita ‘Chikaka, Masika, Mwamba, Chitama Bhagegi’, (shujaa asiyeshindwa). Hawa ni pamoja na Kaya Magha, wananchi wake wakimuita kwa jina la utani kuoneshwa nguvu yake kubwa isiyoweza kushindwa na yeyote, Tunka Manini. Walikuwepo akina Sundiata Keita. Mansa Kankan Mussa, Opuku Ware, Asante Hene huko Assante Empire.  Zote hizi zlianguka kutokana na kujihusisha na masuala ya vita.

Narudia tena kuwa historia haidanganyi. Historia haisemi uongo. Tengeneza fedha. Badala ya kutumia fedha hizo kutafuta amani jifanye unaweza kupigana. Jifanye unaweza kumnyamazisha kila mtu. Utatengeneza mabomu mpaka ya kupuliza kwa mdomo likaenda kuua mtu au kuangamiza Kijiji, lakini vita haitakuacha salama. Utaua wengi. Utanyamazisha wengi lakini iko siku utajuta, utakumbuka nguvu uliyokuwa nayo. Utajikuta umechelewa, wakati huyo wenzako watakuwa wamechukua nafasi. Haya ndiyo yaliwakuta wote. Mobute Tseseseko Kuku Ngembu wa Zagamba huko Zaire, Idd Amin huko Uganda, Tsar Nicolaus huko Urusi ya miaka hiyo.

USA na washirika wake wakumbuke enzi za Uingereza akiwa Bingwa na shujaa wa dunia (Super Power of the World). Historia inasema vita hizi hizi ndizo zilimuondoa katika nafasi ya super power wa dunia. Taifa la Marekani lililochagua kujitenga na vita likachukua nafasi.

Akumbuke kipindi alichopitia Uingerea akijitamba kwamba hakuna saa jua liliwahi kuacha kuangaza ardhi ya uingereza, (The Sun Never Sets on British Empire). Ujumbe huu ulikuwa kweli kwa sababu Uingerea alikuwa ametawanyika dunia nzima. Kama jua linazama Uingereza koloni lake la Afrika mashariki ni mchana. Kama Afrika Mashariki ni usiku koloni lake huko Amerika ilikuwa ni mchana. Huyu ndiye aliyewahi kuifanya Marekani ya sasa kuwa koloni lake. Waingereza wakafanya kosa la kujiingiza kwenye vita ya kwanza na ya pili ya Dunia. Marekani akajitenga, akawa ni muuzaji wa silaha kwa mafahari walioko vitani, walipoishiwa bado akawa ni mkopeshaji mkuuu. Mbinu hiyo iliyopitia katika mpango wa mtaalamu wa uchumi wa Marekani akijulika kwa jina la Marshal (Marshal Plan) ikalifanya taifa la Marekani kuwa kubwa. Baada ya vita, Uingereza bingwa wa dunia badala ya kupambana kuimarisha uchumi wake, akawa na nguvu kubwa kulipa madeni ambayo yalikuwa yakimuendea marekani ambaye alitumia fursa hiyo kuimarisha uchumi wake. Uingereza ikapoteza umaarufu, Akakubali kutoa fursa kwa Marekani. Historia na waswahili tunamwambia Marekani kwamba hakuna marefu yasiyokuwa na ncha.

Iliwahi kuwepo dola ya Kirumi. Hii ilitawala karibia ulaya yote hadi baadhi ya mataifa ya Afrika yaliyoko kaskazini, Misri, Libya na Algeria. Yesu alizaliwa ndani ya dola hii wakati huo wakiwemo magavana mbalimbali kama Ponsio Pilato aliyekuwa akitawala yudea. Jeuri ya Mamlaka na nguvu kubwa kiuchumi ikawapa nafasi ya kutoa hukumu ya Yesu Kuuawa msalabani. Nani aliyeamini Dola ya kirumi itafikia mwisho? Nani aliamini hawa wenye nguvu ya kumhukumu Yesu wangepoteza umaarufu? Vita ikaibua upinzani ndani ya himaya, watu wakagawanyika. Wakashindwa kuwaamini watawala kama ambavyo Wamarekani sasa wanasema angekuwa Trump Marekani Isingeingia kwenye huu mgogoro. Kazi ikawa nyepesi kabisa kwa dola ya Ottoman kuchukua nafasi baada ya kuvamia baadhi ya maeneo ya dola ya Rumi.

NATO wakumbuke nguvu kubwa waliyokuja nayo dola ya Ottoman. Hii iliojitanua. Wakawa mwamba wa dunia.  Sehemu kubwa ya maeneo yaliyokuwa chini ya dola ya Rumi yakawa chini ya Ottoman. Wakasambaa, wakazichukua nchi za Afrika Kaskazini kama vile Libya, algeria, Syria, Misri. Dola ikatanuka hadi kusini mashariki mwa Ulaya kwenye nchi kama hungary, Ugiriki, Ukraine. Ikaenda hadi uarabuni. Ubabe na kujiona wananguvu zaidi, kupenda vita kukaifanya dola hiyo kufikia mwisho, leo hii ni historia.

Ukiangalia katika uhalisia wa dunia inavyokwenda sasa hivi. Marekani ni zaidi ya nchi. Ni dola kubwa duniani. Imetawanya nguvu zake kila sehemu duniani. Imeweka vituo vya kijeshi kila mahali. Imekuwa na nguvu ya kushinikiza masuala mbalimbali yakiwemo ambayo nchi za kiafrika zinayatafsiri kwamba ni kinyume na miongozo ya kimaadili na kidini.

Pamoja na nguvu hiyo ambayo imedumu kwa muda mrefu taratibu mambo yanaanza kubadilika. Nguvu yake ya ushawishi wa dunia kijeshi, kiuchumi, kisiasa, kiutamaduni inaendelea kuporomoka. Wamejigawa kisiasa. Wengine wanaanza kumwelewa Donald Trump kupitia slogan yake ya kwamba ‘Make America Great Again’. Wanaamini kwamba nguvu ya Marekani inaendelea kupotea kila kukicha.

Kidodo kidogo tunaanza kuuona muungano wa kifedha. Mataifa yanaanza kutafuta mbinu za kupunguza utegemezi wa dola. Mataifa kama China, India, Afrika Kusini na Russia wanafikia makubaliano ya kuachana na matumizi ya dola.     Ni suala la muda tu. Historia itaweka wazi tutaanza kusema lilikuwepo dola kubwa la Marekani kama tunavyosema lilikuwepo dola kubwa la Uingereza. Lilikuwepo dola la Rumi.

Comments

Popular posts from this blog

Ujenzi wa Mabwawa kusaidia kuondoa changamoto ya maji Dodoma

Wataalamu Sekta ya maji shirikishaneni maarifa – Naibu Waziri Maji

Katibu Mkuu Wizara ya Maji asisitiza matumizi ya mfumo wa taarifa za sekta ya maji (Maji App)