Wadau wa Sekta Mtambuka watakiwa kuwekeza Zaidi kwenye utunzaji na uhifadhi wa rasilimali za maji


Mwenyekiti Bodi ya Maji ya Taifa Mhandisi Mbogo Futakamba akifungua kikao cha Jukwaa la Taifa la Wadau wa Sekta Mtambuka katika Usimamizi na Uendelezaji wa Rasilimali za Maji kwa Niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Maji Mhandisi Anthony Sanga

Katibu Mkuu Wizara ya Maji Mhandishi Anthony Sanga amelitaka Jukwaa la Taifa la Wadau wa Sekta Mtambuka katika Usimamizi na Uendelezaji wa Rasilimali za Maji kuwekeza Zaidi kwenye utunzaji na uhifadhi wa Rasilimali za Maji ili kuwezesha upatikanajni wa maji kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kijamii na kiuchumi.

Wito huo ameutoa leo kupitia hotuba yake ya ufunguzi wa mkutano wa kwanza wa vikundi kazi vya jukwaa hilo iliyosomwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Maji ya Taifa Mhandisi Mbogo Futakamba jijini Dar es Salaam.

Mhandisi Sanga amesema Serikali inatekeleza sera ya Tanzania ya Viwanda ambayo kwa kiasi kikubwa inahitaji umeme ambao msingi wake mkubwa ni maji.

Picha ya pamoja ya Baadhi ya wajumbe wa Jukwaa la Taifa la Wadau wa Sekta Mtambuka katika Usimamizi na Uendelezaji wa Rasilimali za Maji

“Tanzania ya viwanda inategemea upatikanaji wa umeme wa uhakika na wa gharama nafuu ambao kama mnavyofahamu, umeme unaotokana na nguvu ya maji ni wa gharama nafuu zaidi. Kwa mfano, gharama za uzalishaji umeme wa nguvu za maji shilingi 13 kwa uniti, umeme wa gesi asilia shilingi 129 hadi 153 na kwa mafuta ya dizeli shilingi 546 hadi 675.  Kwa kutambua hilo, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatekeleza miradi mikubwa ikiwemo ujenzi wa Bwawa la Nyerere kwa ajili ya kuzalisha umeme wa maji kiasi cha megawati 2,115 ambapo Mradi huu ukikamilika zaidi ya 70% ya umeme wote nchini utakuwa ni wa maji. Hivyo hatuna budi kuhakikisha rasilimali maji inatunzwa na kuendelezwa” Amesema mhandishi Sanga.


Aidha, ameagiza kila Kikundi Kazi katika jukwaa hilo kiandae Mpango Kazi wa utekelezaji kila mwaka. Pia Mkakati wa utafutaji fedha kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli zilizoainishwa ndani ya Mpango.

Baadhi ya wajumbe wa Jukwaa la Taifa la Wadau wa Sekta Mtambuka wakijadiliana masuala mbalimbali kuhusiana na utekelezaji wa majukumu yao


Jukwaa la Wadau wa Sekta Mtambuka katika Usimamizi na Uendelezaji wa Rasilimali za Maji  limeundwa kwa lengo la kukutanisha Wadau wa Rasilimali za Maji kujadili na kubadilishana uzoefu na ujuzi ili kuboresha utendaji kazi na kuhakikisha usimamizi endelevu wa Rasilimali za Maji kwa maendeleo ya kizazi cha sasa na baadae. Jukwaa hilo lina Wadau zaidi ya 100 wanaotoka katika Taasisi takriban 90 za ndani na nje ya nchi.

 

Comments

Popular posts from this blog

Ujenzi wa Mabwawa kusaidia kuondoa changamoto ya maji Dodoma

Wataalamu Sekta ya maji shirikishaneni maarifa – Naibu Waziri Maji

Katibu Mkuu Wizara ya Maji asisitiza matumizi ya mfumo wa taarifa za sekta ya maji (Maji App)