MIRADI YA MAJI YA UVIKO 19 IKAMILIKE KWA WAKATI-NAIBU WAZIRI WA MAJI MAHUNDI






Naibu Waziri wa Maji Mhandisi Maryprisca Mahundi(Mb) amewataka Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Mkoa wa Simiyu kuhakikisha miradi yote ya Maji inayotekelezwa kupitia fedha zilizotolewa na serikali ikiwa ni Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO -19 inakamilka ifikapo mwishoni mwa mwezi April mwaka huu.

Naibu Waziri,Mahundi amesema hayo  wilayani Busega mkoani Simiyu alipotembelea ujenzi wa tenki la kuhifadhi maji lenye mita za ujazo 50 kwenye mnara wa mita 15  katika kijiji cha Badugu.

Amesema hakuna sababu ya Mkandarasi kushindwa kukamilisha kazi kwa muda huo kwani fedha kwa ajili ya miradi hiyo ipo kinachotakiwa ni kufanya kazi kwa kiwango cha ubora wa hali ya juu na kufuata taratibu za kuomba pesa na kwamba Wizara ya Maji  hawana urasimu wowote juu ya utoaji wa fedha za miradi hiyo.

Aidha, amemtaka Mkandarasi anayetekeleza Mradi huo Kampuni ya Jonta Investiment ya Mjini Shinyanga kufanya kazi usiku na mchana ili mradi ikamilike kwa muda uliopangwa.

"Rais ametoa fedha nyingi kwenye Wizara ya Maji ili kuondoa kadhia kwa wananchi na kufikia azma yake ya kumtua mama ndoo kichwani, hivyo mimi kwa kushirikiana na Waziri wa Maji, Mhe. Jumaa Aweso hatutakubali mtu yeyote kukwamisha miradi",alisema Mahundi.

Awali Kaimu Meneja RUWASA Wilaya ya Busega, Mhandisi Daniel Gagala  akisoma taarifa ya Utekelezaji wa Mradi huo amesema  kiasi cha Sh 317,923,663 zitatumika hadi mradi utakapokamilika.

Amesema hadi sasa kazi zilizofanyika ni pamoja na ujenzi wa tenki, Ujenzi wa vituo tisa vya kuchotea maji, Ujenzi wa nyumba ya mambo na ununuzi wa bomba.

Wizara ya Maji ilipokea jumla ya shilingi Bilioni 139.4 kutokna na Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO -19. Fedha hizo zinatumika kutekeleza miradi ya maji sehemu mbalimbali nchini.

Comments

Popular posts from this blog

Ujenzi wa Mabwawa kusaidia kuondoa changamoto ya maji Dodoma

Wataalamu Sekta ya maji shirikishaneni maarifa – Naibu Waziri Maji

Katibu Mkuu Wizara ya Maji asisitiza matumizi ya mfumo wa taarifa za sekta ya maji (Maji App)